Benchikha apata ushindi wa kwanza Ligi Kuu

KANDANDA Benchikha apata ushindi wa kwanza Ligi Kuu

Na Zahoro Mlanzi • 22:00 - 15.12.2023

Hiyo ni mechi yake ya tatu tangu apewe mikoba hiyo huku akiiongoza timu ya Simba SC katika mechi mbili za kimataifa bila ushindi

Maisha ya Kocha Abdelhak Benchikha, yameanza vizuri ndani ya timu ya Simba SC kwenye michuano ya Ligi Kuu Bara baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Kagera Sugar.

Mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam ni wa kwanza kwa Benchikha ambaye tayari alikiongoza kikosi hicho kwenye mechi mbili za Ligi ya Mabingwa Afrika bila ushindi wowote.

Kiungo mshambuliaji, Saido Ntibazonkiza ndio alikuwa wa kwanza kufungua sherehe za ushindi baada ya kufunga bao la kwanza dakika ya 45 kwa mkwaju wa penatti baada ya yeye mwenyewe kufanyiwa madhambi ndani ya eneo la hatari.

Hata hivyo penalti hiyo ilibidi irudiwe baada ya ile ya awali kupanguliwa na kipa Ramadhan Chalamanda lakini mwamuzi Hans Mabena aliamuru mkwaju huo irudiwe kwa madai kuwa kipa alitoka nje ya mstari.

Bao hilo ilikuwa ndio la pekee kwenye kipindi cha kwamza ambacho kwa muda mwingi kilitawaliwa na Simba.

Kipindi cha pili kilianza kwa kila timu kutafuta bao lakini walikuwa ni Simba ambao walifunga bao la pili safari hii alikuwa ni kiungo Sadio Kanoute akiunganisha kwa kichwa krosi iliyotoka kwa Mohamed Hussein.

Wakati watu wakijua kuwa matokeo yatabaki hivyo nahodha wa Simba, John Bocco aliongeza bao la tatu katika dakika ya 90 akiyatumia vizuri makosa ya mlinzi wa Kagera.

Kwa matokeo hayo Simba, sasa wamefikisha alama 22 wakiwa katika nafasi ya tatu na michezo yao tisa.

Huu ni ushindi wa kwanza kwa kocha Benchikha tangu ajiunge na Simba lakini pia ni ushindi wa kwanza kwa timu hiyo tangu mara ya mwisho walipofungwa 5-0 na Yanga mwezi uliopita.

Tags: