Kocha mpya Simba aanza kazi rasmi

KANDANDA Kocha mpya Simba aanza kazi rasmi

Na Zahoro Mlanzi • 14:30 - 08.11.2023

Cadena ambaye kitaaluma ni kocha wa makipa ndani ya klabu hiyo, amepewa jukumu hilo la kuinoa timu hiyo baada ya kutimuliwa kwa Mbrazil, Roberto Oliveira 'Robertinho

KLABU ya Simba, imeweka wazi kuwa kwa sasa wapo kwenye mikono salama baada ya Kocha wa muda, Daniel Cadena kuanza kazi rasmi ya kuinoa klabu hiyo.

Cadena ambaye kitaaluma ni kocha wa makipa ndani ya klabu hiyo, amepewa jukumu hilo la kuinoa timu hiyo baada ya kutimuliwa kwa Mbrazil, Roberto Oliveira 'Robertinho'.

Robertinho ametimuliwa akitoka kutwaa Tuzo ya Kocha Bora wa Oktoba katika Ligi Kuu Bara, baada ya kufungwa mabao 5-1 na watani zao wa jadi, Yanga.

Akizungumza na Pulse Sports jijini Dar es Salaam, Meneja Habari na Mawasiliano wa klabu hiyo, Ahmed Ally, amesema: “Kocha Daniel Cadena ambaye amekabidhiwa jukumu la kuiongoza timu yetu kwa kipindi hiki ni kocha mwenye wasifu na uwezo mkubwa akimiliki leseni ya juu kabisa ya mpira wa miguu ya Uefa A Licence ameanza kazi.

“Kipindi hiki ambacho tunatafuta kocha mpya timu ipo kwenye mikono salama ndani ya kikosi cha Simba”.

Amewaomba mashabiki wao kuwa watulivu kipindi hiki kwani wanahitaji kuwa wamoja ili kuendelea kutimiza malengo yao ya msimu huu.

Simba kesho itashuka uwanjani kuumana na Namungo FC katika mfululizo wa mechi za ligi hiyo, mchezo utakaopigwa Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Tags: